WANAFUNZI KIGOMA UJIJI WANUFAIKA NA ELIMU YA HAKI ZA BINADAMU
Maafisa wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) kutoka ofisi ya Tabora wakiongozwa na Bw. Raphael Mavunde, wametoa elimu ya haki za binadamu na misingi ya utawala bora kwa wanafunzi wa shule za sekondari zilizopo Manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma tarehe 04 Mei, 2026.
Elimu hiyo imelenga kuwajengea uelewa wanafunzi kuhusu haki zao na wajibu wao, na umuhimu wa kuzingatia misingi ya utawala bora katika jamii.
Aidha, Maafisa hao pia walifanikiwa kufungua Klabu za Haki za Binadamu katika shule za Sekondari Buzebazeba, Masanga na Mwananchi kwa lengo la kuendeleza uelimishaji na kujenga utamaduni wa kuheshimu haki za binadamu miongoni mwa wanafunzi.
Klabu hizo zinatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa wanafunzi kujadili masuala ya haki, uwajibikaji na uongozi bora.
Akizungumza wakati wa shughuli hiyo, Bw. Mavunde amesisitiza umuhimu wa wanafunzi kutumia klabu hizo kama nyenzo ya kujifunza na kushiriki kikamilifu katika kulinda na kutetea haki za binadamu.
Ameleza pia kuwa vijana ni msingi wa jamii yenye haki na utawala bora, hivyo wanapaswa kupewa maarifa sahihi mapema ili wawe raia wema na wenye uwajibikaji.

