DK. MWINYI AWAHAKIKISHIA WAFANYAKAZI KUPATA HAKI ZAO MSINGI.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amewahakikishia Wafanyakazi kupata stahiki na haki zao za msingi kwa Mujibu wa Sheria za Utumishi na kanuni ziliopo Zanzibar.
Dkt. Mwinyi ameyasema hayo kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Kizimkazi, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.
Amesema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatambua na kuthamini kazi kubwa inayofanywa na wafanyakazi kwa kuleta mageuzi makubwa na kukuza uchumi na ustawi wa jamii kwenye sekta mbalimbali za maendeleo kupitia ushirikiano uliopo baina ya Serikali na vyama vya wafanyakazi.
Dk. Mwinyi ametoa wito kwa vyama vya wafanyakazi na waajiri nchini kuungana na Serikali kuhakikisha haki zote za msingi za mfanyakazi zinalindwa ili kujenga ufanisi na uwajibikaji kwenye maeneo yao ya kazi.
Pia, Dk. Mwinyi amewataka wafanyakazi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu, nidhamu na uzalendo kwa kuwa walinzi wa amani na utulivu uliopo nchini hususan kuelekea Uchaguzi Mkuu Mkuu kwa amani na kulinda maslahi ya Taifa. Huku wakizingatia kuchagua viongozi waadilifu.
Watumishi wa Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora (THBUB) Ofisi ya Zanzibar ni miongoni wa watumishi walishiriki kwenye maadhimisho hayo ya siku ya wafanyakazi duniani 2025, yaliyoadhimishwa kwa kauli mbiu isemayo "Uchaguzi Mkuu 2025, Utuletee Viongozi Wanaojali Haki na Maslahi ya Wafanyakazi, sote Tushiriki”