THBUB YAWAHAMASISHA WAZAZI NA WALEZI KUHESHIMU HAKI ZA WATOTO

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imewahimiza wazazi, walezi na jamii yote kwa ujumla kuhakikisha wanawalinda watoto dhidi ya utumikishaji wa watoto katika shughuli za kiuchumi ikiwemo biashara, kilimo na ujasiriamali.
Kauli hiyo imetolewa na Mchunguzi Mkuu Msaidizi Bw. Paul Sulle alipokuwa akitoa elimu ya haki za mtoto kwa wazazi , walezi na watoto waliotembelea banda la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, lililoko kwenye maonesho ya ya Kimataifa ya 49 ya Biashara maarufu kama Sabasaba Jijini Dar es salam Julai 7,2025.
Bw. Sulle alieleza kuwa wazazi wana jukumu la msingi katika kuhakikisha watoto hawashiriki katika kazi zinazohatarisha afya, usalama, au kuathiri makuzi na maendeleo yao kielimu.
“Wazazi hawapaswi kuchukulia biashara kama nafasi ya kuwahusisha watoto katika kazi nzito au hatarishi kwa kisingizio cha kusaidia familia. Ulinzi wa haki za Mtoto ni wajibu wa kila mzazi, mlezi na Jamii kwa ujumla,” alisema Bw. Sulle.
Aidha aliongeza kuwa baadhi ya watoto nchini hujikuta wakifanyishwa kazi kwenye biashara ndogondogo kama kuuza bidhaa mitaani au sokoni wakiwa katika umri mdogo, bila kujali usalama wao wala haki yao ya kupata elimu na kuwa hali hiyo ni kinyume na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto na sheria ya Mtoto nchini.
Tume inashiriki maonesho ya Sabasaba kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora, kutoa ushauri wa kisheria na kupokea na kushughulikia malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bor