ELIMU YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA YATOLEWA KWA WANAFUNZI MLEZI.
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), imetoa elimu kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mlezi iliyopo Jijini Dodoma, Septemba 16, 2026.
Akizungumza wakati wa kutoa elimu hiyo, Afisa wa THBUB, Bw. Innocent Rweyemamu, amesema elimu hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi msingi mzuri wa kuwa raia wanaoheshimu sheria, wanaowajibika, wanaotoa na kupokea taarifa kwa uwazi pamoja na kushiriki katika masuala mbalimbali yanayowahusu.
“Wanafunzi ni viongozi wa kesho, sisi kama THBUB tuna wajibu wa kuwapatia elimu hii,” amesema Bw. Rweyemamu.
Bw.Rweyemamu amesema kuwa uwazi ni miongoni mwa maingi wa utawala bora, ambapo wanafunzi wamefundishwa umuhimu wa kusema ukweli, kutoa taarifa sahihi na kutoficha jambo ambalo ni muhimu kwa wengine kulifahamu.
‘’katika mazingira ya shule, uwazi unaweza kuonekana pale mwanafunzi anapotoa taarifa sahihi kuhusu changamoto inayomkabili, pamoja na viongozi wa wanafunzi na walimu kutoa taarifa kwa uwazi kuhusu mambo yanayowahusu wanafunzi’’amesema Bwa.Rweyemamu.
Kwa upande wake, Afisa wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Bw. David Piniel alitoa elimu kuhusu haki muhimu za binadamu na kueleza kuwa haki ya kuishi ni miongoni mwa haki za binadamu inahusisha kupata mazingira salama yanayomwezesha kuishi na kukua, huku haki ya kulindwa ikihusisha ulinzi dhidi ya ukatili, unyanyasaji na vitendo vinavyoweza kumdhuru mtoto. Aidha, ameeleza kuwa haki ya kupata elimu ni muhimu katika kumwezesha mtoto kupata maarifa na ujuzi wa kujenga maisha yake na kutimiza ndoto zake.

